Afisa Vijana, Ndugu Kassim Toto, Februari 14, 2026, amekutana na Maafisa Usafirishaji wa Halmashauri ya Mji wa Mbulu na kuwahimiza kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku, sambamba na kuwa chachu ya kuwahamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.
Katika kikao hicho, alisisitiza umuhimu wa kushirikiana na Maafisa Maendeleo ya Jamii ili kupata mwongozo sahihi kuhusu taratibu za kuomba mikopo ya vijana, akieleza kuwa mikopo hiyo ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha vijana kujiajiri, kupunguza ukosefu wa ajira na kukuza uchumi wa familia na jamii.
Aidha, Ndugu Toto aliwahimiza vijana kutumia ubunifu, nidhamu na mshikamano katika kuanzisha na kuendesha miradi ya uzalishaji mali, pamoja na kuzingatia uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali wanazopata ili kuhakikisha miradi yao inakuwa endelevu.
Ameongeza kuwa ushirikiano mzuri kati ya maafisa wa sekta mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha vijana wanapata taarifa sahihi, wanajengewa uwezo na wanapata fursa za kujikwamua kiuchumi na kuchangia maendeleo ya taifa.
Kwa upande wao, Maafisa Usafirishaji walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani ili kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wa barabara, huku wakihimizwa kuwa mabalozi wa usalama huo katika maeneo yao ya kazi.

Copyright ©2020 GWF . All rights reserved.