


Diwani wa Kata ya Sanubaray, Mhe. Emmanuel Lohi, ametoa wito kwa wananchi, walimu na wanafunzi kushiriki kikamilifu katika upandaji na utunzaji wa miti kama hatua muhimu ya kulinda mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Mhe. Lohi ameyasema hayo leo Februari 10, 2026, wakati wa zoezi la upandaji miti lililofanyika katika Shule ya Msingi Guwangw, ikiwa ni muendelezo wa kampeni ya upandaji miti katika taasisi za Serikali, pamoja na kuunga mkono jitihada za Serikali katika uhifadhi wa mazingira na rasilimali za asili.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Lohi alisisitiza kuwa upandaji miti si tukio la siku moja, bali ni mchakato endelevu unaohitaji usimamizi, ufuatiliaji na utunzaji wa karibu ili miti hiyo iweze kukua na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.
“Tunapanda miti ili kutunza mazingira yetu yanayotuzunguka. Ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha miti hii inatunzwa vizuri, kwani itatusaidia kuboresha hali ya hewa, kuzuia mmomonyoko wa udongo na kuimarisha afya ya jamii yetu,” alisema Mhe. Lohi.
Aidha, aliwahimiza walimu kuendelea kuwajengea wanafunzi utamaduni wa kupenda na kutunza mazingira tangu wakiwa wadogo, akieleza kuwa elimu ya mazingira ni msingi muhimu wa maendeleo endelevu ya Taifa.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Guwangw,Mwl. Saymon Kissimbi,ameahidi kusimamia ipasavyo utunzaji wa miti hiyo kwa kushirikiana na walimu na wanafunzi, ili kuhakikisha inakua na kuleta tija katika mazingira ya shule. Ameeleza kuwa zoezi hilo limekuwa funzo muhimu kwa wanafunzi kuhusu uwajibikaji na umuhimu wa kulinda mazingira.
Jumla ya miti 70 imepandwa katika Shule ya Msingi Guwangw, ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa juhudi za kuhifadhi mazingira na kuimarisha uoto wa asili katika Kata ya Sanubaray.
Zoezi hilo linaendelea katika taasisi mbalimbali za Serikali na linatarajiwa kuongeza mwamko wa jamii kuhusu umuhimu wa upandaji na utunzaji wa miti kwa maendeleo endelevu.
Copyright ©2020 GWF . All rights reserved.