



Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amewataka Madiwani wa Wilaya ya Mbulu kuwa mstari wa mbele katika kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika maeneo yao, akisisitiza kuwa uongozi wao upimwe kwa uwezo wa kuleta suluhisho la changamoto zinazowakabili wananchi.
Ameyasema hayo leo, Februari 12, 2026, wakati akifungua mafunzo ya siku mbili kwa Madiwani yaliyofanyika kuanzia Februari 11 hadi 12, 2026, yakijumuisha Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Mbulu na Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Mhe. Sendiga alieleza kuwa Madiwani ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wananchi, hivyo wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za Halmashauri pamoja na misingi ya utawala bora.
Aliwahimiza kufanya mikutano ya mara kwa mara na wananchi kwa kuzingatia vipaumbele vya maendeleo, ili kusikiliza changamoto zao na kupanga mipango ya utekelezaji kwa pamoja.
“Rudini kwa wananchi wenu, sikilizeni kero zao na zipatieni ufumbuzi. Msikubali kuwa sehemu ya malalamiko; kuweni sehemu ya suluhisho,” alisisitiza Mhe. Sendiga.
Aidha, aliwataka Madiwani kujiwekea malengo mahsusi katika utekelezaji wa shughuli za Serikali na kuhakikisha wanakuwa wasimamizi madhubuti wa maendeleo katika kata zao.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri ili kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Aliwataka Madiwani kuwa wabunifu katika kubuni na kupanua vyanzo vipya vya mapato, pamoja na kusimamia rasilimali zilizopo kwa ufanisi, uwazi na uadilifu.
Mhe. Sendiga alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kusisitiza uwajibikaji, usimamizi thabiti wa rasilimali za umma na utoaji wa huduma bora kwa wananchi. Hivyo, aliwataka Madiwani kwenda kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uzalendo na kujituma ili kuendana na dhamira ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo endelevu.
Mafunzo hayo yamelenga kuwaimarisha Madiwani katika misingi ya uongozi na utawala bora ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya uwakilishi na usimamizi wa maendeleo ya wananchi.
Copyright ©2020 GWF . All rights reserved.