Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Mhe. Michael Semindu, amewaagiza watendaji wote wa Serikali kuhakikisha suala la bima ya afya kwa wote linakuwa agenda ya kudumu katika jamii.
Ameyasema hayo Januari 05, 2026 wakati akifungua mafunzo ya bima ya afya kwa wote yaliyotolewa kwa viongozi wa dini, madiwani na watumishi wa Halmashauri ya Mji wa Mbulu.
Mhe. Semindu ameeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anatarajiwa kuzindua mpango wa bima ya afya kwa wote mwezi Januari.
“Bima ya afya kwa wote iwe agenda ya kudumu katika vikao vyote vitakavyofanyika, kwa sababu ni moja ya ahadi ambazo Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliahidi kutimiza ndani ya siku 100 baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Mhe. Semindu.
“Ili kuunga mkono juhudi za Serikali, tunatakiwa kuhakikisha elimu juu ya umuhimu wa bima ya afya kwa wote inawafikia wananchi wa Mbulu,” aliongeza Mhe. Semindu.
Kwa upande wake, Mratibu wa Bima ya Afya Mkoa wa Manyara, Dkt. Charles Shija, ameeleza kuwa bima ya afya kwa wote itatolewa kwa kaya ikihusisha baba, mama na watoto.
“Serikali imedhamiria kuhakikisha Watanzania wanapata matibabu bila kuumizwa na gharama, ndiyo maana imeanzisha bima ya afya kwa wote itakayogharimu shilingi laki moja na nusu (150,000/=) kwa mwaka mzima,” alisema Dkt. Shija.
Dkt. Shija aliongeza kuwa bima ya afya itatoa nafasi kwa kaya maskini na watu wenye ulemavu.
Mwisho, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Mbulu, Dkt. Adrianus Kalekezi, aliahidi kuendelea kufanya ufuatiliaji ili kuhakikisha elimu juu ya bima ya afya inatolewa kwa wananchi
Copyright ©2020 GWF . All rights reserved.